Follow us

VITA VYA KIROHO : ROHO ZITAWALAZO MAENEO

Tangazo




Katika makala hii tutaangalia mafundisho yanayohusiana na kile wanachokiita “Roho za Kimaeneo”. Kulingana na mafundisho hayo, wanadai kuna roho chafu maalum ambazo zinatawala jamii, vijiji, miji, jiji au hata nchi nzima. Hiyo ina maana kwamba, roho hizo zinatawala katika eneo zima kulingana na jiografia ya eneo lenyewe; na hivyo huitwa “Roho za Maeneo”. Inaendelea kufundishwa zaidi kwamba eti hizi roho za maeneo zanao uwezo na mamlaka ya kuwabana watu katika giza, vifungo na dhambi kulingana na jiografia ya eneo lao. Kimsingi, zaidi ya hilo, hawa wanaohamasisha mafundisho hayo, wanatuambia kwamba hizi roho za maeneo zinao uwezo wa kushikilia jamii ndogo au miji kiasi kwamba Injili peke yake haiwezi kufaa, kupata kuingia wala kupendwa au kuenea katika eneo hilo hadi hapo hizi roho za kimaeneo zitakapotambulikana na kisha zikafungwa, zikazidiwa nguvu pamoja na kukemewa kwa njia ya maombi. Wanafundisha kwamba watu hawawezi kumjia Bwana, wakaokolewa na kukombolewa kutoka katika dhambi, giza, pamoja na vifungo mbalimbali, kwa idadi kubwa mpaka kwanza hapo tutakapotambua na kisha kuzifunga na kukemea nguvu za roho hizo za kimaeneo. Hivyo ndivyo wanavyosema na kuwafundisha watu.

Hiki ndicho kidokezo cha mafundisho yao kwa lugha rahisi kadiri iwezekanavyo, na nina hakika kwamba utakubali kuwa ikiwa mafundisho haya ni ya kweli, basi ni ya umuhimu mkubwa. Kuenea kwa Injili pamoja na kuokolewa kwa watu kunategemea ufahamu na matumizi ya mafundisho haya, ikiwa mafundisho hayo ni ya kweli! Jambo hili haliwezi kuwa swala la jinsi mtu aonavyo au tafsiri ya kibinafsi, kwa sababu litaathiri ufahamu wetu kuhusiana na jinsi Injili ilivyo, pamoja na lile alilolifanya Yesu pale Kalvari.

Kama ilivyo katika zile makala nyingine zilizopita, napenda kwanza niangalie yale ambayo Maandiko yanavyosema na kufundisha. Kwa hivyo, kwa muda huu, hatutaangalia Maandiko ambayo watu wanadhani wamepata kuyaona mambo hayo yakifundishwa. Jambo hili ni la msingi na lenye uzito mkubwa kiasi kwamba hatuwezi kuyaachia kwenye ubunifu au hisia za kibinadamu tu. Tunachotafuta ni maandiko ambayo mambo haya yanafundishwa dhahiri na kutajwa bayana.

Mambo haya yanafundishwa wapi ndani ya Agano Jipya?

Kwa jibu la urahisi na la ujumla kuhusiana na habari hiyo hapo juu ni – “Hakuna popote!” Hatuyapati mahala popote katika Agano jipya, mafundisho haya yahusuyo kutambua na kuzifunga roho za kieneo!

Yesu hakutumia au kufundisha mbinu hii.

Hakuna mahali popote tunaposoma kuwa Yesu aliibainisha roho iliyokuwa ikitawala eneo, kijiji au mji, na kisha akaifunga na kuikemea kabla hajaanza kuhubiri na kufanya miujiza mahali hapo.

Hakuna mahali popote ambapo Yesu aliwafundisha mitume wake au mtu mwingine yeyote kwamba Neno la Mungu linaweza kuwa na nguvu na mafanikio katika eneo fulani ikiwa kwanza utaibainisha roho ya lile eneo na kuifunga na kuzishinda nguvu zake kwa njia ya maombi. Kamwe hatusomi popote Yesu akiitumia au kuifundisha mbinu hii.

 Mitume hawakutumia au kufundisha mbinu hii.

Hakuna mahali popote pale katika Injili au kwenye Matendo ya Mitume ambapo tunasoma habari za mitume au mtu mwingine yoyote yule akitumia mbinu za jinsi hiyo katika kuineza Injili. Mtume Paulo alitembelea miji mingi sana ambamo kulikuwa na zinaa ya kutisha, mambo ya kimwili, uchawi pamoja na dhambi. Hakuna popote pale ambapo tunasoma juu yake akizitambua kwanza roho hizo katika miji hiyo ili aone ni aina gani ya roho za kimaeneo zinazotawala katika miji, wala hatusomi mahala popote pale na kuona akiomba juu ya roho za aina hiyo ili kwamba kazi ya Injili ipate kustawi.

Hakuna mahali popote pale ndani ya maandishi yao kwa makanisa au kwa watu binafsi, ambapo mitume hawa wamepata kutaja tu mbinu za jinsi hiyo, licha ya kuzifundisha. Yapo mahusia mbalimbali kwa ajili ya kuomba katika Agano Jipya. Lakini hakuna mahali popote pale ambapo mitume wanaelekeza kuwa roho za kimaeneo zina uwezo juu ya watu katika baadhi ya maeneo na kwamba watu hawana budi kuomba dhidi ya roho hizo na kuzivunja nguvu zake, ili kwamba Injili ipate kustawi na ili wanawake na wanaume wapate kuokolewa.

Hayapo mafundisho ya jinsi hiyo ndani ya Agano Jipya. Kwa msingi huu pekee, tunaweza, kwa usalama kabisa, kuyakataa mafundisho ya jinsi hii.

Lakini sasa, mtindo wa jinsi hii haufudishwi kwenye Agano la Kale wala hatuna hata mfano mmoja katika Agano la Kale, unaoelezea juu ya mtu yeyote anayezitambua roho za kimaeneo na kufunga nguvu zake kabla kazi ya Bwana haijakamilishwa ipasavyo. Kwa kweli, waandishi hao wa kisasa wanarejea katika maandishi fulani fulani ya Agano la Kale, na tutakwenda kuangalia maandishi hayo baadaye, lakini hata hivyo, hakuna hata andiko moja linalounga mkono mtindo huo na mbinu zao zinazoenezwa na waandishi hao.

Jukumu la Uongo

Wanawezaje walimu hawa wa siku hizi kusema, “Lazima uzitumie mbinu hizi ili kuhakikisha mafanikio ya uInjilisti katika ulimwengu”, wakati ambapo maandiko hayatushauri kufanya hivyo? Wanaweka jukumu juu ya watu we Mungu wakati ambapo maandiko hayaweki jukumu la jinsi hiyo. Kwa maneno mengine, wao huongezea maneno yao juu ya Neno la Mungu – na wakizitumia mamlaka zao juu ya watu wa Mungu, mamlaka ambazo hazitokani na Mungu. Hili ni jambo la hatari sana. Ni jambo moja kusema kuwa, kwa sababu maandiko hayawazuii kuzitumia mbinu hizo, kwa hivyo wao wanajisikia uhuru kuzitumia. (Hata hivyo, hoja hii si ya msingi, kwa sababu mafundisho yao yanagusa kweli za msingi za Injili na ufanisi katika kuenezwa kwake, hivyo wanapaswa kuonyesha kwa uhakika mambo hayo yanafundishwa wapi katika maandiko, kabla hawajafundisha na kuzitumia kanuni hizo). Lakini kwa kweli wanafundisha kanuni zao za lazima kwa ajili ya kueneza Injili. Huo ni udanganyifu na unaweza kuwapelekea watu wa Mungu, kutumbukia katika kuchanganyikiwa, vifungo pamoja na hatari iwapo watapokea na kuyafuata mafundisho ya jinsi hii.

Ikiwa mbinu hizi za kuzitambua na kuzifunga roho za kimaeneo ni za lazima kwa ajili ya kuleta mafanikio ya uenezaji wa Injili, kwa nini basi Yesu pamoja na mitume wake hawakufundisha wala kutufunulia mambo hayo? Tunaelezwa na hawa walimu wa kisasa kwamba maombezi dhidi ya mamlaka na uweza juu ya maeneo ya kijiografia, yanahitajika sana kabla Injili haijapenya katika maeneo hayo. Je, mitume walikuwa ni wajinga juu ya mbinu hizo? Au labda walishindwa kutufunulia kile kilicho cha lazima kwa ajili ya uenezi wa Injili, na kwa ajili ya wokovu wa nafsi za watu? Je kanisa litakuwa limeondolewa ukweli huu wa lazima kwa muda wa miaka 2000? Hapana! Kanisa halijanyimwa ukweli huu wa lazima, na bado Injili imeendelea kuenea muda wote huo kwa karne zote hizo, kama Yesu alivyosema Injili haina budi kuenea, hata bila kanisa kufundisha au kuzitumia mbinu hizo ambazo hawa walimu wa kisasa wamezibuni. Kutokea muda wa Matendo ya Mitume hadi kufikia siku hii ya leo, kumekuwepo na uamsho, maelfu ya watu wamerejea kwa Bwana kwa idadi kubwa, nao wameokolewa kutokana na dhambi, giza na vifungo vya shetani pasipo hata kujulikana kwa mbinu hizo, kufundishwa wala kuzitumia!

Kutamani “matokeo” kupita kiasi.

Lakini moja ya kusudio lao kuu hawa wahubiri na walimu wa kisasa ni kuona “matokeo”. Mmoja wa viongozi wa kanisa ambaye anaamini katika kutumia kanuni hizo amesikika akisema kuwa iwapo kanisa lake halitaongezeka kutoka washirika 1000 hadi kufikia washiriki 2000 ndani ya miaka miwili, basi hapo itakuwa ni kutokana na kushindwa kwao katika kujaribu kwa makini kufanya hivyo. Kwa maneno mengine, iwapo tutazitumia mbinu halisi basi tutegemee kanisani washirika kuongezeka mara mbili zaidi ndani ya miaka miwili! Watu hawa wanalifanya kanisa kuwa kana kwamba ni aina fulani ya biashara ambapo tunapaswa kuzitafuta kanuni bora zaidi ili kutoa matokeo na kufikia malengo. Hata makanisa mengi kwa sasa yameanza kutoa “maelezo ya umisheni” pamoja na malengo yao kwa ajili ya mafanikio yao. Mtindo wa aina hii kwa kazi ya Mungu, umeazimwa moja kwa moja kutoka kwa ulimwengu wa kibiashara. Hii yote inamdhalilisha Yesu Kristo ambaye ndiye kichwa cha kanisa lake ambaye ndiye aliyetuonyesha kwa neno lake jinsi itupasavyo kujishughulisha wenyewe. Mmoja wao amesema kwa uwazi kabisa kwamba wanavutiwa zaidi na yale “yanayofanya kazi” ( yaani, yanayoleta mafanikio au matokeo ) kuliko “yale yaliyo ya kweli”. Kwa hiyo basi, tayari wameanza kujenga msingi wa udanganyifu wao. Katika kujiondoa kwao kutoka katika miongozo iliyo sahihi ya Neno la Mungu, wao wamekuwa wakijiweka wazi kwa udanganyifu wa shetani; kadiri wanavyoendelea na kuzitumia mbinu na kanuni zinazoweza kuwaletea matokeo ya haraka na yenye kuvutia.

Yesu anaomba kwa Baba akisema “Neno lako ni kweli”, Yohana17:17. Sasa kama watu wa Mungu, sote tunatamani na kuomba kwamba Injili iweze kufikia na kuokoa nafsi za watu wengi watuzungukao na ulimwenguni kote. Lakini watu wa Mungu, maombi yetu, kazi zetu, pamoja na mafundisho yetu lazima yawe kulingana na neno la Mungu, ambako ndiyo kweli. Hamu yetu ya “kuona matokeo” isituongoze kuelekea kwenye kuikataa au kujitenga na Neno la Mungu kama lilivyofunuliwa katika maandiko; au kuanzisha mbinu zetu wenyewe au mtindo wa fikra kwa ajili tu ya kujipatia kile kinachoonekana kuwa ni “matokeo” ya haraka. Mengi ya mafundisho hayo ya kisasa yanasukumwa na mawazo ya “mafanikio” yakikusudia kutafuta kitu fulani “kinachofanya kazi” na hiyo ni “Mafanikio”. Hawa walimu wa kisasa wanaendelea kubuni mawazo mapya pamoja na mitindo ya kufundisha. Hakuna hata mmoja anayeweza kujihoji mwenyewe kuwa inakuwaje kila baada ya miaka michache kunahitajika “mitindo” mipya, katika mtazamo wa Kitheolojia – hii ni upepo mpya wa imani! Wala hakuna hata mmoja anayeweza kuuliza, kulitokea nini na ule upepo wa imani uliopita? Au kutambua kwamba kanisa halihitaji mtindo mpya katika mafundisho yake ya Imani isipokuwa ni marejeo kwa yale ambayo tayari yamefunuliwa vizuri katika maandiko. Ikiwa tutakuwa waaminifu, tutapaswa kuungama kwamba, mafundisho hayo mengi ambayo yanaendeshwa na wazo la mafanikio ni matokeo yanayotujia moja kwa moja kutoka kwenye mila za kibiashara za Marekani (U.S.A); mahala ambako kila kitu kinategemea malengo, matokeo pamoja na mafanikio. Na Wakristo zaidi sana huko Marekani wameazima akili hizo au wamechukua mtazamo na silka kutoka kwa ulimwengu na wameuingiza kanisani, umewapelekea kwenye ubunifu wa mafundisho na matendo ya kutatanisha.( Bila shaka, mimi sisemi kwamba, wazo la roho za kimaeneo linakuja kutoka kwenye desturi za kibiashara, lakini huu msukumo kwa ajili ya mafanikio – ambao umewapelekea Wakristo hawa kutumbukia katika ubunifu na udanganyifu).

Mwandishi na mwalimu ambaye ni mmoja wa waenezaji wakuu wa mafundisho haya anaelezea juu ya jambo ambalo nimeligusia hapo juu, kuhusiana na kukosekana kwa maandiko yanayounga mkono mafundisho haya. Katika utangulizi wa kitabu chake alichokiandika yeye mwenyewe kiitwacho “Territorial Spirits” (“Roho za Kimaeneo”; Sovereign World Ltd. Ó1991 C.P.Wagner), amesema kuwa, amewahi kutazama kwenye vitabu 100 huko kwenye seminari ya theolojia ambavyo vimezungumzia kuhusiana na somo la malaika na mapepo, ili aweze kugundua mafundisho yahusuyo roho za kimaeneo. Anaendelea kueleza kuwa, siku za leo ipo haja kubwa sana ya kufanya utafiti kwa ajili ya somo hilo. Lakini kwa nini tufanye utafiti? Je utafiti wa kwenye Biblia hautoshi? Je hatuna Biblia? Neno la Mungu halitoshi kutuelekeza kuhusiana na jambo kama hili la msingi? Kwa dhahiri kabisa sivyo hivyo, kwa kuwa yeye hawaaliki watu wafanye utafiti katika Biblia. Ijapokuwa kwa hakika anajaribu kutafuta ushahidi kwa ajili ya mafundisho hayo kwenye maandiko, kama tutakavyoweza kuona hapo baadaye, yeye anaenda sehemu nyingine ili kuona iwapo anaweza kupata uthibitisho kwa ajili ya ubunifu huu wa kigeni. Lakini anatuambia kwamba ni vitabu vitano tu kati ya 100 vilivyotaja kuhusiana na somo hilo la roho za kimaeneo, na kati ya hivyo vitabu vitano, ni vitatu tu ambavyo angalau vinasema chochote kinachoweza kusaidia. Lakini hakuna chochote kati ya vitabu hivyo ambacho kilistahili kujumuishwa katika kitabu chake. Hii haishangazi kwa vile mafundisho hayo hayamo pia katika Biblia – na mpaka sasa hakuna hata mmoja ambaye amebuni au kuyatumia kwa jinsi hiyo, kwa kadri nifahamuvyo. Kwa hiyo, katika kitabu chake hicho anajumuisha michango kutoka hasa kwa waandishi wa siku za leo ambao wanaoeneza mawazo ya jinsi hiyo. Wagner alikuwa anafanya utafiti juu ya kanuni za ukuaji wa kanisa na maombi, alipowafikia viongozi wa kanisa fulani ambao walikuwa wakifanya aina hii ya maombezi dhidi ya roho za kimaeneo. Hapo, ilimpelekea kuingia ndani zaidi ya mafunzo yake juu ya somo hili. Kama tulivyokwisha kuona katika makala nyingine iliyopita, watu hao wanapofanya utafiti wao hawaanzi kwa kusoma Biblia, isipokuwa wao huanza kwa kutegemea uzoefu wao wenyewe na “mafunuo ya kiroho” wanayoyapokea. Ndipo hutafuta maandiko ambayo huyalazimisha au kuyafanya yaunge mkono “mafunuo” waliyopokea. Nasi tutatazama maandiko hayo hapo baadaye. Lakini napaswa kusema kuwa, hata hao viongozi wa makanisa – ambao waliiamini imani hiyo ya kigeni, hawakubaliani wao kwa wao kuhusiana na mafundisho haya, na namna ambayo yanapaswa kutumiwa. Kwa vile hayaungwi mkono na maandiko ya Neno la Mungu, basi haishangazi kuona kwamba mmoja wa waenezaji wa mawazo haya ameamua kusema kwamba kwa kuwa Mungu ni mwenye enzi, basi anafunua mbinu mpya na bora kwa ajili ya uInjilisti wa ulimwengu mzima. Wanachomaanisha ni kwamba Mungu anaufunua kwao ufunuo huu usiopatikana katika Biblia, na hivyo wanajihesabia wenyewe mamlaka ya kitume! Yote hii inaonyesha jinsi wanavyoiacha imani, kwa vile wanayainua mafununuo yao na uzoefu wao juu ya neno la Mungu.

Hebu sasa tuyatazame kwa karibu yale yanayofundishwa na waandishi hawa wa kisasa kuhusu vita vya kiroho.

Mafundisho yao juu ya Vita vya Kiroho.

Wanaigawa vita ya kiroho katika ngazi tatu. Kwanza, kuna kile wakiitacho mapambano ya “ngazi ya chini”, ambayo wanamaanisha kutumia mamlaka ambayo Mungu amelipatia kanisa lake kuwatoa mapepo toka kwa mtu mmoja mmoja. Hii imetolewa mfano wake vizuri katika Injili na Matendo ya Mitume na hivyo siyo jambo lenye kuleta hoja kwetu. Aina ya pili inaitwa mapambano ya “ngazi ya kishirikina” ambavyo wanamaanisha kuwa ni kukabiliana na kuzifunga roho za uchawi, dini ya kishetani, ibada za sanamu, na kadhalika, mambo ambayo kwa kawaida yanaleta athari zake ovu kupitia kwa mtu fulani binafsi. Ngazi ya “juu” ya mapambano ya kiroho inaitwa mapambano ya “kimkakati” au ya “kwenye anga za juu” ambapo maombezi yanahitajika ili kuzitambua na kuzifunga roho mbaya za ngazi za juu, au mamlaka na nguvu, ambazo zinatawala katika maeneo makubwa ya kijografia.

Hizi ngazi mbili za mwisho ni mambo ya kukisia na ubunifu wa hawa waandishi wa kisasa, kama tutakavyoweza kuona. Ile ngazi ya pili haina umaarufu mkubwa na inaingiliana kwa kiasi fulani na ile ya tatu. Kwa hiyo nitazungumza kidogo juu ya ngazi hii ya pili, tutakapoangalia vifungu vinavyohusiana nayo. Lakini ni ngazi ile ya tatu ambayo mafundisho yao yanakazia, kwa hiyo kwa upana zaidi tutakuwa tunatazama ngazi ya mwisho, kwa vile ndiyo hasa inayowakilisha udanganyifu na hatari kubwa.

Ni namna gani roho hizi mbaya zinatambulikana na watu kukabiliana nazo? Sawa, kwa wale ambao wanaamini kuwa wameitwa ili kuhusika na aina hii ya vita, wanatumia muda wao mwingi katika maombi kutafuta kutambua kwa njia za karama za kiroho na “upambanuzi”, jina au aina ya roho (moja au zaidi ya moja) iliyoshikilia eneo fulani – inaweza ikawa ni roho ya kiburi, uchoyo, tamaa mbaya au uchafu, ndipo tena wanakabiliana nayo katika vita vya maombi na kuzifunga nguvu zake – hii inaweza ikachukua siku kadhaa au wiki kadhaa. Ili kutambua ni roho gani inatawala juu ya mji, wanafundisha pia haja ya kile wanachokiita kuwa ni “kutengeneza ramani za kiroho”, kazi ambayo inahusisha uchunguzi wa historia ya mji – hali ya mji huo kidini, kijamii na kikabila, na historia ya nyuma, hali kadhalika kuhusu matendo maovu yaliyofanywa katika mji huo, au kufanywa na mji huo, au yaliyofanywa dhidi ya mji huo – kurudi nyuma miaka zaidi ya mia au kama si elfu na zaidi! Inafundishwa kwamba tendo hili litatusaidia sana kuzitambua ni roho chafu za jinsi gani zinazoshikilia mji kwa nguvu sana ili kwamba tuweze kuomba kwa ufanisi dhidi yake na kisha kuzifunga nguvu zake! Nilishughulikia juu ya hoja hii ya kiushirikina katika ile makala yangu ya kwanza.

Baadhi ya hawa wahubiri wa kisasa wanasema kwamba hawataweza kuhubiri Injili katika eneo lolote lile hadi kwanza wawe wametambua roho mbaya zinazotawala na wakazifunga nguvu zake. Lakini sasa Yesu hakutumia mtindo huu katika mji wowote aliouendea. Hatusomi chochote kuhusiana na mtume Petro au Paulo akishiriki katika aina hii ya “vita vya kiroho” kabla hajautembelea mji wowote ule; au kuhubiri Injili hapo. Hatusomi chochote kile kuhusiana na mtume Paulo kuzifunga roho za uzinzi, uchoyo au tamaa mbaya kule kwenye miji ya Efeso au Korintho kabla hajaanza kazi yenye nguvu hapo. Wala hatusomi popote kwamba katika nyaraka zao kuwa mitume hao waliwasihi watakatifu kuomba dhidi ya roho za kimaeneo, kama hawa waandishi na wahubiri wa kisasa wanavyotutaka sisi tufanye!

Makosa Mawili ya Kimsingi

Fundisho hilo siyo tu kwamba ni nyongeza kwa Maandiko, bali kwa kweli linaielezea vibaya na kuidhoofisha kazi yote ya Kristo pale Kalvari na jinsi Injili ilivyo. Na tutaanza kwa kuyatazama makosa mawili ya kimsingi ambayo mafundisho hayo yanawatumbukiza watu ndani yake.

Kwanza, fundisho hili linakanusha au kupunguza ushindi mkamilifu ambao Yesu aliutimiza pale msalabani. Mafundisho yenyewe hauyakiri kikweli ushindi halisi ambao Kristo ameupata dhidi ya nguvu zote katika ulimwengu wa roho, kwa niaba ya kanisa lake, kadhalika na kwa ajili ya wanadamu, wala hawa walimu hawaheshimu kikweli na kujali mamlaka zote na haki ambazo Mungu anazo za kuwaelekezea watu wake na kujenga kanisa lake.

Kabla ya pale Kalvari, Yesu mwenyewe alikuwa akitembea huko na huko akihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu. Hali kadhalika aliwatuma mitume pamoja na wanafunzi kuhubiri Injili ya ufalme wa Mungu na kuwatoa watu mapepo na kuwaponya wagonjwa. Akiwa amepokea msamaha na ushindi juu ya majeshi ya uovu pale msalabani, Kristo aliita, akatuma na akawatumia mitume vile vile na watu wengine katika kulijenga kanisa lake. Tunajua kuwa watu wengi waliokolewa kupitia mahubiri ya mtume Petro. Filipo alitumwa na Mungu kuwageuza wengi watokane na dhambi na uchawi. Matendo 8. Na katika ile Matendo 11:19-21, tunasoma kuwa, “… mkono wa Bwana ukawa pamoja nao, wao … waliohubiri Yesu ni Bwana kwa mataifa na watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana”. Mtume Paulo aliitwa na Mungu, Matendo 26:13-18; katika ile Matendo 13:2 mtume Paulo alitumwa na Mungu. Watu hawa wote walihubiri neno la Mungu kwa watu wengine, wakikiri kile ambacho Kristo amekifanya pale Kalvari na watu wengi walimgeukia Bwana. Mitume waliwakomboa waume kwa wake pia kutokana na roho za uovu na waliyakemea mapepo yaliyokuwa yakitenda kazi ndani ya mtu mmoja mmoja. Matendo 13:8-11; 16:18; 19:12. Hayo yote yalitokea pasipo hata kupata mafundisho yahusuyo na pasipo matumizi ya mtindo huu wa kisasa ambao unaitwa “mapambano ya kimkakati”

Hebu niseme hapa kwamba inapaswa iwe wazi kwetu, kwamba sio mahubiri yoyote na kila mahubiri huwa na ufanisi. Mtume Paulo alikuwa makini katika kumhubiri Kristo, lakini yeye alijikabidhi mwenyewe kwa ndugu zake pamoja na kwa kanisa, naye alikuwa tayari kurejea nyumbani kwake katika mji wa Tarso, Matendo 9:26-31. Baadaye tunamkuta kama mmoja wa manabii na walimu huko Antiokia, Matendo 13:1. Paulo hakuhubiri tu mahali popote pale kulingana na mipango yake na ubunifu wake, bali akiwa na ushirika na Mungu na akimtii Roho na kanisa, Paulo aliitwa na Mungu kuihubiri Injili, Matendo 13:1, na alielekezwa na Roho maeneo ya kwenda na maeneo ya kutokwenda, Matendo 16:6 – 10. Hivyo mtume Paulo anasema katika Warumi 10:14 – 15. “…basi wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikiaje pasipo mhubiri? Tena wahubirije wasipopelekwa?” Mtume Paulo pamoja na wenzake walikuwa makini sana kuhusiana na wito huu wa kimungu – 1 Kor. 9:16,17 na alikuwa makini zaidi pia kuwa angeweza kufanya kazi vizuri tu kulingana na wito wake, 2 Kor. 10:13-18.

Ikiwa tutaenda mbali na wito wa Kimungu na karama; ikiwa tutaenda mbali na muda wa Kimungu katika maisha yetu; ikiwa tutaenda mbali na Neno la Mungu – basi tusitegemee kupata matunda ambayo Mungu anayategemea kutoka kwetu. Tunapaswa kuwa watumishi wa Mungu, hii ina maana kwamba tunatakiwa kufanya yale tu anayoyasema na kujikabidhi kwenye maelekezo yake na muda wake katika maisha yetu. Hatutakiwi pia kwenda mbali zaidi ya karama na wito wetu. Hii inaweza kuwa pengine ndiyo sababu wengine wanaenda pasipo kupelekwa? Inaweza kuwa ndiyo sababu kwamba wanapata mafanikio kidogo au hawaoni mafanikio kabisa kutokana na mahubiri yao. Juhudi ya jinsi hii ya wahubiri wasio na subira wanatafuta sasa kutunga au kubuni mtindo fulani au mbinu ambazo zitaifanya kazi yao iweze kufanya kazi vizuri na kuleta “mafanikio”! Inaweza ikawa ndiyo sababu wanaenda mbali zaidi ya yale ambayo yanafundishwa na Maandiko ili kwamba wapate haya? Ninafikiri kuwa mambo hayo pia yanachangia katika jambo hili lote la UInjilisti wenye mafanikio pamoja na kushughulikia “mbinu mpya”. Hii yote haimaanishi kuwa ikiwa tumetumwa na Mungu, basi siku zote tutaona ‘matokeo makubwa’, bali ikiwa tuna shauku ya kumtumikia Mungu na kumzalia matunda na kiukweli kupeleka Neno lake kwa watu, basi tutaenenda kwa kufuata Neno lake na Roho wake.

Kama tusomavyo Injili na Matendo ya Mitume, tunaona kwamba watu wa Mungu walihubiri na kushuhudia juu ya kifo chake na ufufuo katika utii wa amri zake na maongozi yake au kwa kadiri fursa zilipojitokeza. Ijapokuwa walifahamu kuwa Kristo ameangamiza mamlaka na uwezo, haina maana yoyote, kama tusomavyo katika habari zao, kwa watu wa Mungu kuchukua UInjilisti “katika mikono yao wenyewe” na kujaribu kuifanya kazi ya Mungu kwa ajili yake. Mitume hawakufanya mambo kwa kukisia pale walipokuwa wakilitumia neno la Bwana au walipotumia uwezo na mamlaka ambazo aliwapatia. Walimtii Mungu na Mungu aliwarejesha wengi kwake na akadhihirisha nguvu zake kuu. Na Mungu aliupata utukufu! Hayo yote yalitendeka pasipo hata kuzitambua au kuzifunga roho za kimaeneo! Hawakujaribu kuongezea chochote kile juu ya yale ambayo Mungu alisema na kuyafanya ili kuufanya uInjilisti uwe wenye mafanikio zaidi! Lakini hawa walimu wa kisasa pamoja na wahubiri wanathubutu kuonyesha kwa mafundisho yao, kwamba yale ambayo Kristo aliyafanya pale msalabani hayakutosha. Ndiyo, wanatangaza kwamba Kristo alipata ushindi pale msalabani, lakini inaonekana kana kwamba hakuzivunja mamlaka na enzi vya kutosha kwa ajili yao, kwa sababu wahubiri hawa wanaamini kuwa roho chafu bado zina haki kisheria kuwashikilia watu katika giza na kifungo na kuwa Injili haiwezi kupenya katika eneo linalotawaliwa na roho hizo. Wanafundisha kuwa mtu anahitajika kwanza kufanya “vita vya kiroho” ana kwa ana na mamlaka hizo pamoja na nguvu hizo kwa maombi, hadi kuzishinda nguvu zake kupitia maombi kwanza, kabla Mungu hajazirejesha roho za watu kwake! Mawazo ya aina hii kwa hakika ni ya jamii ya kiushirika tu na yenye milki ya ulozi zaidi kuliko kuwa na mawazo ya kimaandiko. Mtazamo huu juu ya aina hii ya roho ya kimaeneo pamoja na uwezo wao pamoja na aina hii ya kuzingatia katika maombi dhidi ya roho ya uovu, hayapatikani katika maandiko ya neno la Mungu. Mtazamo huu unaweza kumtukuza ibilisi kwa namna itakayowanyima watu wa Mungu ufahamu wa kweli na nguvu ya Kristo ndani ya watakatifu wake na kupitia kanisa lake. Inawafanya watu wamfikirie shetani zaidi badala ya kuweka mawazo yao kwa Kristo, na kwa jinsi hiyo wanampatia shetani uwezo zaidi na utukufu na kuwanyang’anya watakatifu ile imani yao ya kweli katika Mungu. Maandiko yanasema kwamba, “Ijapokuwa hatujayaona mambo yote yakitiishwa chini ya nyayo zake, lakini tunamwona Kristo.” Amina! Lakini sasa, badala yake walimu hawa wa kisasa wanatutaka sisi tuyaone mapepo! Ni mafundisho madhaifu na manyonge kama vile yenyewe yalivyo si ya kibiblia. Na hao walioyahamasisha mafundisho hayo ndio huwa wa kwanza kukubali katika vitabu vyao kwamba watu wameharibiwa walipokuwa wanajaribu kutumia mbinu hizo. Mafundisho hayo ni kashfa dhidi ya mamlaka ya Mungu na shambulizi dhidi ya ushindi kamili wa Kristo alioupata pale Kalvari, ambao ndio unaomruhusu kulijenga kanisa lake kulingana uradhi wa mapenzi yake mwenyewe. Katika uweza ambao Mungu aliutumia katika kumfufua Kristo kutoka katika wafu. (Efe 1: 19-23)!

Ndiyo tunatambua kile kinachofundishwa na maandiko, kwamba mfalme wa uweza wa anga ni ile roho itendayo kazi sasa katika wana wa uasi; Efe 2:2. Shetani huzungukazunguka kama simba angurumaye akiwafunga wengi kuyatenda mapenzi yake na hafanyi lolote isipokuwa ni kuua, kunyang’anya na kuharibu. Yeye hudanganya na kuwafunga wengi katika vifungo. Mambo hayo pamoja na mengineyo yanafundishwa ndani ya maandiko, na wala hiyo sio hoja yetu tena hapa. Nami sisemi hapa kwamba hatuwezi kuomba kwa Mungu, kuhusiana na mambo ya aina hii; wakati ambapo tunajua hali na watu ambao wanahitaji neema ya Mungu, rehema pamoja na wokovu wake. Lakini linapokuja jambo la uenezi wa Injili na jinsi inavyoenezwa na kubadilisha maisha ya watu, ndipo tunaweza kusema kuwa mafundisho hayo ya kisasa yameenda nje ya maandiko, na yametumbukia katika kasoro na udanganyifu – yanawafanya watu wawe shabaha ya roho za udanganyifu. Wanakubali kuwa Kristo amepata ushindi pale kalvari dhidi ya shetani, lakini bado wanaamini kwamba wanatakiwa pia wapate ushindi zaidi juu ya roho zinazotawala ju ya maeneo yote yanayokaliwa na watu.

Ni nini kinaipatia roho hizo za kimaeneo haki ya kisheria kukamata mamlaka za aina hii juu ya watu, kiasi kwamba hata iifanye Injili isiwe yenye mafanikio katikati yao? Haya ati wanasema ni zile dhambi zilizopita za jumuia hiyo au mkoa na ile laana iliyowekwa juu yake kwa sababu ya dhambi hizo! Napenda niwaambie ukweli, wanachokifanya hawa walimu wa kisasa ni kuzijaza akili za watu wa Mungu mambo yasiyo ya kiInjili yenye ushirikina mtupu na yenye kasoro nyingi. Kristo amezichukua dhambi za ulimwengu mzima na amelipia gharama kubwa isiyohesabika ili kufanya hayo. Kristo ni mwenye mamlaka zote za juu – ni Mkuu. Shetani anaweza tu akaenda pale ambapo Mungu amemruhusu kwenda. Sawa, maandiko yanakiri kuwa ipo haja ya maombi, kuhubiri, uInjilisti, kazi pamoja na ukombozi wa mtu mmoja mmoja kutokana na mapepo; lakini kadiri ya haja ya kuihubiri Injili inavyohusika, bado maandiko hayakiri kwamba kuna haja ya toleo lingine zaidi ya lile alilolinunua tayari Kristo pale msalabani kwa ajili ya ulimwengu wala maandiko hayakiri kwamba “dhambi zile za kihistoria” zilizopita za maeneo ndizo zinaipatia roho za kimaeneo haki ya kisheria kuzuia Injili; wala pia maandiko hayakiri kuwa ipo haja ya watakatifu kujiingiza moja kwa moja katika makubaliano ya kiroho na hizo roho za kimaeneo kana kwamba roho hizo zinahitajika kufungwa kabla ya Injili kufanyika na kuenezwa kwa mafanikio yanayopaswa ( tafadhali angalia makala yangu ya kwanza ambamo jambo hili limeelezwa kwa undani zaidi ).

Wakati mtume Paulo alipokuwa Athene, hawakupatikana watu wengi waliomgeukia Mungu lakini pamoja na hali hiyo, si Paulo mwenyewe wala si maandiko ya Neno la Mungu yanapohesabu hali hiyo ya watu kutoipokea Injili kuwa ilisababishwa na nguvu kuu na mamlaka au haki ya roho za uovu kupinga Injili au kazi ya Mungu. Mtume Paulo hakuianza kuzishughulikia roho za kimaeneo katika maombi kwa sababu ya kuonyesha “upungufu wa mafanikio” katika huduma yake. Mtume Paulo alikuwa na ufahamu mkubwa zaidi na mafunuo kuliko hawa walimu wa kisasa, lakini yeye hakukimbilia kwenye “mbinu za kiwango cha kimkakati” ili kuzishinda “roho ya kuabudu sanamu” ambazo zilidhaniwa “kutawala” katika mji wa Athene, katika jitihada yake ya kuushinda upungufu huu wa mwitikio katikati ya watu. Unaona, hawa walimu wa kisasa wao wanasema kwamba, watu kwa kweli hawapo huru kuitikia Injili hadi hapo tutakapokuwa tumezifunga roho za kimaeneo! Mmoja wa waandishi, kwa kweli anapendekeza kuwa roho za kimaeneo zinazotawala kule Athene, zilikuwa zenye uwezo mkubwa kiasi kwamba zilimfanya mtume Paulo kuzishindwa na eti hiyo ndiyo sababu alipata mafanikio kidogo sana huko! Lakini sio Paulo wala maandiko ya neno la Mungu yanayohitimisha jambo hilo kuhusu aina hii ya “upungufu wa mafanikio”. Badala yake, mtume Paulo yeye anaendelea mbele na safari yake kwa mapenzi yake Mungu na mpaka anapoingia katika mji wa Korintho, hatuoni popote pale panapomuonyesha akijishughulisha na kazi ya kuzifunga roho za kimaeneo, na bado watu wengi sana walimgeukia Bwana. Maandiko hayaelezei sababu hasa inayofanya watu wengi zaidi wamgeukie Bwana katika eneo moja kuliko jingine, lakini yanatupa vidokezo na kutuelekeza kwenye kanuni fulani fulani, ambazo tutaziangalia hivi punde.

Lakini jambo moja lenye uwazi ni kwamba maandiko hawayahesabii “mafaniko” au “kupungua kwa mafanikio” kwamba imetokana na mtu mmoja ambaye ameweza kuzishinda roho za kimaeneo zinazotawala au la.

Ninadhani kuwa kama hawa walimu wa kisasa wangekuwepo kule nyakati zile za Paulo alipotembelea Athene, wangeweza kushauri kuwa Paulo aweze kuhudhuria masomo katika moja ya seminari ya Kithiolojia ili aweze kujifunza kwanza “kanuni za kukua kwa kanisa”. Pengine wangeweza kumwelezea pia kuwa mtindo wake anaoutumia katika UInjilisti bila shaka “haufanyi kazi” vizuri na hivyo anapaswa kuzisomea “mbinu mpya za mafanikio” ya uenezaji wa Injili, ambazo ndizo zimethibitishwa kuleta mafanikio! Wangeweza kumwambia kuwa yote aliyoyafanya amekosea kwa sababu tatizo halikuwa ni Wathene binafsi isipokuwa ni ile roho ya kieneo ya kuabudu sanamu ndiyo iliyokuwa inawazuia watu kule wasiweze kuiitikia Injili. Mtume Paulo angelazimika kufundishwa vita vya kiroho iwapo angependa kuona mafanikio katika kuieneza Injili! Angepaswa kujifunza kuhusu kutambua majina ya roho chafu za kimaeneo na namna ya kuzikabili katika kuzifunga kwa maombi! Asingetazamia kupata mafanikio hadi kwanza afahamu jinsi ya kuyafanya mambo haya! Lakini sasa hebu fikiria jinsi Paulo alivyoweza kuwashughulikia walimu wa uongo walionyemelea makanisa ya Galatia; sifikirii kwamba angeweza kuvutiwa kwa vyovyote vile, badala yake angeweza kuwakemea kwa nguvu kwa ajili ya kuichafua Injili ya Kristo.

Hii ndiyo sababu inayonifanya niseme kwamba, mafundisho hayo wanayotuletea ni kashfa dhidi ya mamlaka na busara za Mungu, ambaye huwaita na kuwatuma watu kwenda kuhubiri Injili kulingana na amri na mafundisho ambayo ameyaweka kwa ajili yetu. Hawa waandishi wa kisasa wanaweka busara yake Mungu na mamlaka za utawala wake katika maswali. Wangeweza kuiita huduma ya Paulo kwa ajili ya watu wa Athene ni jambo “lililoshindwa”. Wako makini kutafuta mafanikio kiasi kwamba wanadiriki kuisukumilia mbali amri ya Kristo – ya kwenda ulimwenguni kote kuihubiri Injili – sasa kinyume chake wao wanazunguka huku na huko wakianzisha amri zao wenyewe, na hivyo wanajiweka kinyume na busara za mamlaka ya Mungu na utawala wake juu ya mambo haya.

Hata kama Mungu alibariki au kama aliwaruhusu waweze kujaribiwa, hata kama kulikuwa na mwitikio mkubwa wa watu au kidogo – bado mitume wa mwanzoni kabisa, wao pamoja na kanisa waliendelea kumwangalia Mungu; wakijikabidhi kwake, wakimwamini yeye na kumtukuza yeye! Hivyo ndivyo walivyofanya! Na kama hapakuwepo na mwitikio sana, hawakumtilia shaka Mungu na kuanza kukimbia huko na kuko kujifunza na kubuni “kanuni mpya za ukuaji wa kanisa”! Wao walikuwa wakiomba na wakihubiri na walikuwa imara katika imani na upendo; kama vile tusomavyo katika kitabu cha Matendo ya Mitume, lakini wao pia hawakujishughulisha katika aina ya maombi yanayohusika na kuzishambulia roho za kimaeneo kama ambavyo inavyohamasishwa na waandishi hawa wapya.

Ijapokuwa wanakiri juu ya ushindi wa Kristo pale Kalvari, lakini mafundisho yao hayo yanaufanya wokovu wa roho za watu uonekane kuwa unategemea matokeo ya aina fulani ya mapambano ya ana kwa ana kati ya majeshi ya kiroho ikiwepo roho chafu kwa upande mmoja, ikipambana na karama za Roho na maombezi ya Wakristo kwa upande mwingine; vita hiyo inayoelezwa humo ni ubunifu wa akili zao wenyewe tu ( ambayo wanaiazima kutoka kwenye milki za ulozi. Vitabu vya ubunifu – kama vile kitabu cha Frank Perret ) na vinajaribu kuongezea kitu kingine juu ya ushindi ambao Kristo aliupata pale Kalvari (msalabani). Katika maandishi yao, wakati mwingine inatolewa mfano wa nguvu za upinzani zilizo sawa sawa zikipigana dhidi ya roho. Wanaonyesha kuwa iwapo hutazishinda roho za kimaeneo zilizo za kienyeji na za kimaeneo zinazomiliki eneo fulani, basi kazi ya Injili na wokovu wa nafsi haiwezi kufanikiwa ipasavyo. Katika kutimiza hamu yao ya kupata “mitindo ya mafanikio”, wahubiri hawa pamoja na waandishi wao hawajikabidhi katika Neno la Mungu na maelekezo yake ambayo Yesu ameyakamilisha pale msalabani – wanafanya hayo yote kwa ajili tu ya kutafuta matokeo. Nasema tena kwamba mawazo hayo ni ya kuanzishwa toka duniani, hayamtukuzi Mungu, badala yake yanatukuza mafundisho yasiyothibitishwa ambayo husababisha machafuko na kukata tamaa, na zaidi ya yote yanamtukuza shetani.

Mafundisho yasiyothibitishwa ambayo husababisha kuchanganyikiwa na kukata tamaa.

Lakini hebu niseme hapa kuwa shauri lao halijathibitishwa! Bila shaka haionyeshi kwamba wanaweza kwa kweli kuonyesha kuwa jamii imebadilishwa kutokana na mafundisho hayo yao. Zaidi ya hayo yote, wengi wa mashabiki wa mafundisho hayo wanaishi Marekani (USA). Je huko kwao yameleta mabadiliko gani? Mchungaji mmoja wa kanisa moja kubwa kule New York aliwahi kuandika kitabu kuhusu kazi za kanisa lake na jinsi Mungu alivyopambana na mafundisho haya ya kisasa – na jinsi hata yeye alivyoumizwa katika moyo wake kuona jinsi ambavyo dhana hii isiyo ya kibiblia inavyoweza kushikilia akili za watu wa Mungu na inaendelezwa kufundishwa nchi nzima. Lakini analiweka swali lile lile na linalofanana – kuelezea ni kwa nini basi, iwapo mafundisho hayo ni ya ukweli, mbona hayabadilishi miji ya Amerika – tunaambiwa na watu wengine kuwa California ya kusini ni mji unaowakilisha kituo cha vivutio vya matamanio katika ulimwengu. Yako wapi basi mabadiliko hayo makubwa katika miji ya Marekani iwapo mafundisho hayo ni ya ukweli? Lakini mtu mwingine anaweza kuuliza hivyo hivyo kuhusu miji mingine mingi pamoja na nchi. Mafundisho hayo hayo yamekuwa yakiendeshwa Uingereza karibu miaka 15 sasa kwa kadiri ninavyofahamu, lakini sasa, yako wapi – basi mabadiliko hayo makubwa yaliyoahidiwa na mafundisho hayo? Ninafikiri kuwa watu wengi wangekubali kwamba, sio jamii tu yenye hali mbaya, isipokuwa kanisa leo limo katika hali mbaya zaidi; kwa kusema kwa ujumla, liko katika hali mbaya kuliko ilivyokuwa miaka 20 iliyopita. Tendo mojawapo lililosababisha machafuko, matengano, maumivu ya mioyo, kuchanika kwa makanisa, kadhalika na kugawanyika kwa makanisa, je huko ndiko kuzaa kwa wingi kwa imani hiyo mpya!

Mashabiki wa mafundisho hayo wametengeneza mkanda wa video, ili kuwashawishi watu waone namna ambavyo vita hivyo vya kiroho vinavyoleta mafanikio. Baadhi ya watu wengine ambao wamechunguza yale yanayodaiwa na mikanda hiyo ya video, kwa kuzuru hadi kwenye maeneo hayo waliyo chukulia mkanda huo pamoja na kupata habari sahihi za maeneo hayo, wanatuambia kuwa mambo mengi, yaliyodaiwa ndani ya mikanda hiyo yametiwa chumvi – na mara nyingi ni habari za uongo. Wale wanaoamini katika imani au mafundisho hayo, kwa uasili wa kutosha wanaamini kwamba “inafanya kazi” na wanajaribu kuonyesha watu kuwa ni kutokana na mtindo wao mpya wa kuomba dhidi ya roho za kimaeneo, ndiyo iliyoleta mafanikio makuu pale Injili ilipobanwa katika jumuiya fulani fulani. Lakini hatuoni kuungwa mkono na maandiko ya Neno la Mungu katika maeneo hayo; na wala haiwezi ikaonyeshwa kuwa hilo limekuwa ndiyo “ufunguo” au “jawabu” la ufanisi wa uInjilisti kwa namna ya kimatendo, mbali ya malalamiko ya hadithi zao.


Kwa kweli kitabu kimeandikwa ambacho nimekitaja hapo punde tu, kwa usahihi kabisa ni kwa sababu kumekuwepo na machafuko pamoja na maumivu ya moyo yaliyosababishwa na mafundisho hayo. Mwandishi wa kitabu hicho yeye mwenyewe pia anaamini katika vita vya kiroho dhidi ya roho, lakini anatueleza kuhusiana na kukata tamaa pamoja na hofu iliyowanyemelea wakristo waliokuwa na matazamio ya hali ya juu ya mafanikio kutokana na mafundisho hayo. Lakini hatimaye waligundua kuwa haikufanya kazi yoyote; ile kama walivyotarajia na hata ikawasababishia majanga! Hali hiyo imewasababishia kujisikia ni watu wawezao kunaswa na shida, hofu na machafuko! Ingawaje anajaribu kuonyesha kuwa mambo yaliwaharibikia kwa sababu ya ongezeko na ujinga wa watu wenyewe wa kutokujua kanuni za aina hii ya mapambano; mbali ya hayo yote kitabu hicho pia kinakazia ukweli kwamba, upepo huu mpya wa imani sio huo ambao mashabiki wake wamelalamikia kuwa ndio, na wala hautoi matokeo kwa namna ambayo hawa waandishi wapya wangetupelekea sisi tuamini hivyo.

Post a Comment

0 Comments