Askofu wa
Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Kardinali Polycarp Pengo amewataka
wananchi kumuunga mkono Rais John Magufuli katika kufufua uchumi.
Akihubiri
wakati wa ibada ya mkesha wa Krismasi jana Jumapili Desemba 24,2017 katika
Kanisa la Mtakatifu Maurus lililopo Kurasini, Kardinali Pengo amesema wananchi
wamuunge mkono Rais kwa kufanya kazi badala ya kuwa walalamikaji.
"Magufuli
na wasaidizi wake tuwaunge mkono kwa kufanya kazi kwa bidii ili kujiletea
maendeleo," amesema.
Kardinali
Pengo amesema watu wanapofanya kazi kwa bidii nchi inakuwa na amani ambayo
ndiyo msingi wa maendeleo.
"Wakati
umefika wa watu kufanya kazi usiku na mchana, hilo likifanyika nchi itaendelea
kuwa na amani. Muda wote uwe wa kufanya kazi bila kujali ni usiku au mchana,
tupumzike kidogo kwa ajili ya kupata usingizi," amesema.
Kardinali
Pengo amesema amani ya kweli duniani haitokani na viongozi waliopo madarakani
bali wananchi wenyewe.
Amesema kila
mtu afahamu kwamba chimbuko la amani ni kufanya kazi halali inayopendeza
machoni mwa Mungu.
Amewataka
wananchi kuliombea Taifa na viongozi wake ili waendelee kusimamia ujenzi wake.
0 Comments