Kocha Mkuu wa Yanga Sc, Miguel Gamondi amesema kila mchezaji aliye ndani ya kikosi cha Yanga Sc ana umuhimu na ubora, huku akisisitiza kuwa mchezo wa leo dhidi ya Medeama utaendelea kuibua maswali kwake nani aanze na yupi asubiri kutokana na idadi ya wachezaji wanaoanza.
Yanga Sc licha ya mastaa wake wengi kukosa
namba kikosi cha kwanza, wengi wako kwenye levo nzuri ya ubora na wana utimamu
wa miili, hivyo hicho ndicho kinampa jeuri ya kuona kila mchezaji ni staa
kikosini.
Gamondi amefunguka hayo siku moja baada ya
kutoa nafasi kwa wachezaji ambao wamekuwa wakikosa namba kikosi cha kwanza
kucheza kwa ubora ndani ya dakika 90, wakiipa timu hiyo ushindi wa mabao 4-1
dhidi ya Mtibwa Sugar.
“Siwezi kumzungumzia mchezaji mmoja mmoja. Nachoweza kusema Yanga ina wachezaji wengi wazuri na bora, lakini idadi ya wachezaji wanaotakiwa kuanza ni 11, hivyo napata wakati mgumu nani aanze kulingana na ubora lakini lengo la wote ni kuona timu inasonga mbele,” - alisema.
“Juzi kulikuwa na mabadiliko mengi kikosini
na hiyo imetoa mwanga namna Yanga ilivyo bora na inanipa mtihani wa kupanga
kikosi. Nafurahishwa na hilo na najivunia kuongoza timu inayonipa matokeo bila
kujali nani yupo na nani hayupo.”
Gamondi alisema wamesahau matokeo dhidi ya
Mtibwa Sugar na sasa akili zao zimehamia kimataifa wakiamini bado wana nafasi
ya kufanya vizuri huku akiweka wazi kuwa matokeo waliyopata yameongeza morali.
“Tumecheza mechi tatu bila matokeo mazuri
kimataifa, kushinda kwenye ligi na kupata idadi kubwa ya mabao ni moja ya njia
sahihi kuwarudisha wachezaji mchezoni,” alisema.
“Kuhusu mwendelezo wa wachezaji waliotumika
dhidi ya Mtibwa Sugar kucheza kesho hilo kama kocha nitaliamua baada ya mazoezi
ya mwisho kwani mchezaji ni binadamu – leo anaweza kuwa mzima na bora kesho
ikawa tofauti.”
Gamondi alisema ushirikiano na ubora
ulioonyeshwa na mastaa wake anatamani kuona unaendelea kimataifa ili
kujihakikishia kucheza robo fainali jambo ambalo linawezekana wakipambana na
kutumia vyema uwanja wa nyumbani kwa mechi mbili walizonazo.
Kesho Yanga Sc itaialika Medeama kwenye Uwanja
wa Mkapa ikiwa na kumbukumbu ya kuambulia sare ugenini baada ya kufungana bao
1-1.
0 Comments