Follow us

SAFARI YA SIAH MALLE KATIKA UHANDISI INAVYOIBUA VIPAJI VIPYA VYA WANAWAKE WENYE NDOTO KUBWA

Tangazo

 

Na Mwandishi Wetu

Siah Malle ni mfano mzuri wa mwanamke ambaye amefanikiwa kuvunja dhana iliyojengeka na kuwagawa wanawake na wanaume kwenye uwanja wa taaluma mbalimbali duniani. Safari yake ya kuwa jaji katika Kongamano na Maonesho ya 8 ya Wanawake Wahandisi Tanzania (TAWECE) ni uthibitisho tosha kuwa ari na bidii yake katika tasnia ya uhandisi imezidi kumuinua.

Alipokuwa anakua, Siah alivutiwa na ulimwengu wa sayansi na teknolojia. Kaka yake ambaye ni mhandisi wa ujenzi, alichochea shauku yake katika kuingia kwenye tasnia ya uhandisi na alidhamiria kufuata nyayo zake.

Lakini pia kwa kutiwa moyo na walimu wake, alisoma sayansi na hisabati katika elimu ya sekondari na kufanikiwa kufaulu vizuri katika masomo hayo.

Baadaye Siah aliendelea na elimu yake katika kozi ya uhandisi ngazi ya stashahada ambayo alisoma kwa muda wa miaka mitatu katika Chuo cha Ufundi Arusha.

Mmoja wa walimu wake aliyefahamika kwa jina la John Mbando, alitambua uwezo wake mapema na kumtia moyo katika fani hiyo kisha kumshawishi kuachana na uhandisi wa ujenzi na kubobea katika uhandisi wa mitambo.

Mbando alimshawishi kuwa uhandisi wa mitambo kuwa una manufaa mengi, ikiwa ni pamoja na kuajiriwa, manufaa na kubuni vitu mbalimbali ambavyo vinatatua changamoto au matatizo yanayoikumba jamii.

Hali hiyo ilisababisha mapenzi ya Siah katika uhandisi wa mitambo kuongezeka na alidhamiria kuingia katika taaluma hii.

Baada ya kuhitimu vizuri stashahada yake, Siah alisoma kwa miaka mitatu katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya ambako alihitimu Shahada ya Kwanza ya Uhandisi Mitambo na kupata alama zenye wastani wa (GPA) 4.3 na kutunukiwa tuzo ya Mwanafunzi Bora wa Kike aliyehitimu mwaka wa kuhitimu 2019.

Mwalimu wa Siah, Mbando ndiye aliyefanikisha safari muhimu ya mwanadada huyu ambaye sasa ni mhandisi mbobevu.

Hakumfundisha tu ujuzi wa kiufundi wa uhandisi wa mitambo, lakini pia alimjengea dhima nzima ya umuhimu wa kuzingatia maadili, mawasiliano na kufanya kazi kwa pamoja.

Alimhimiza kufuata ndoto zake na kamwe asikate tamaa, hata anapokabiliwa na changamoto. Uzoefu wa Siah ni ushuhuda wa nguvu ya ushauri na athari ambayo mwanamke au mtu yeyote anaweza kuwa nayo kwenye kazi na maisha ya kila siku.

Baada ya kumaliza masomo yake, Siah aliajiriwa na kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) kwa ajili ya mafunzo ya ufundi mitambo kama mhandisi wa mitambo.

Leo, anafanya kazi kama Mratibu 2 – katika idara ya inayoundwa na timu ya wahandisi. Anafurahi kuwa sehemu ya kampuni hiyo inayojitolea kuwajibika kwa kwa jamii kwa namna mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwajengea uwezo zaidi wafanyakazi wake bila kujali jinsia huku ikiendelea na shughuli za uchimbaji madini mkoani Geita.

Katika GGML, Siah amepata fursa ya kufanya kazi katika miradi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kubuni na kutekeleza ufumbuzi wa nishati endelevu.


Post a Comment

0 Comments